Tuesday , 1st Dec , 2015

Msanii Joh Makini ambaye ametokea mji wa Arusha amesema wasanii wengi ambao wanatoka nje ya Dar es salaam wanafanya vizuri kwenye fani kwa sababu ya majukumu yanayowakabili.

Joh Makini ameyasema hayo alipokuwa akiongea kwenye kipindi cha Mkasi kinachorushwa na East Africa Television, na kusema kuwa wao kama wasanii ambao wanakuja kutafuta maisha jijini Dar es salaam wanalazimika kujituma zaidi ili kuweza kumudu gharama za maisha zilizopo, tofauti na ukiwa nyumbani.

 

“Kuwepo mbali na nyumbani lazima ukaze ili uweze ku-sustain, kulipa kodi na mambo mengine ukiwa ugenini, ndiyo sababu inayowafanya wasanii kutoka mbali kukaza wakifika dar es salaam”, alisema Joh Makini.

 

Pamoja na hayo Joh Makini amezungumzia suala la wasanii wa Nigeria kuwepo wengi ambao wanafanya vizuri mpaka kimataifa wakati hapa nyumbani wakiwa wachache, na kusema wingi wa watu waliopo nchini mwao na kuwepo kwa lebo za muziki, ni moja ya sababu inayofanya wasanii wengi wa nchi hiyo wawe juu.

 

“Nigeria wana watu wengi ujue, kwa hiyo wana uwezo wa kuuza kopi milioni nchini mwao tu, na pia  wana record lebel, kwa hiyo haiwezi kuwa nchi ya mastaa wachace, wanazalisha vipaji vingi kutokana na hizo record lebel”, alisema Joh Makini.

 

Ili kukabiliana na tatizo hilo Joh Makini amesema anakusudia kuifanya kampuni ya weusi kuwa lebo ya muziki siku moja, ili iweze kuinua vipaji na wasanii wachanga na kukuza sanaa ya Tanzania.

 

“Nataka weusi iwe kubwa na kuwa na recording lebel, iweze kuwafanyia recording na kuinua vipaji vya wasanii wachanga”, alisema Joh Makini.