Thursday , 30th Mar , 2017

Waziri Mkuu wa Ethiopia Mhe. Hailemariam Dessalegn anatarajiwa kuwasili nchini Tanzania kesho Machi 31 na kufanya ziara ya kitaifa ya siku mbili ikiwa ni mwaliko wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli.

Rais Magufuli akisalimiana na Waziri Mkuu wa Ethiopia Hailemariam Desalegn wakati akitoka kwenye mkutano wa wakuu wa nchi za Afrika uliofanyika hivi karibuni nchini Ethiopia

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa Mhe. Suzan Kolimba amesema dhumuni la ziara hiyo ni kukuza uhusiano mzuri uliopo baina ya Tanzania na Ethiopia pamoja na kujadiliana fursa zaidi za ushirikiano katika maendeleo mbalimbali ikiwemo uwekezaji na biashara.

Naye Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia Bi. Naimi Azizi amesema Ethiopia imejizatiti katika kukabiliana na changamoto ya tatizo la umeme hususani katika bara la Afrika na kwa sasa inatekeleza mradi mkubwa wa umeme ambao unaweza kusaidia baadhi ya nchi za Afrika.