Saturday , 21st Jun , 2014

Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu Philemon Luhanjo ameshauri kuwepo kwa mafunzo maalumu kwa wafanyakazi wanaokaribia kustaafu ili kuwajengea uwezo wa kukabiliana na maisha mara baada ya kustaafu kulitumikia taifa.

Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu Philemon Luhanjo.

Luhanjo alitoa kauli hiyo jana wakati wa uzinduzi wa mpango maalumu wa kutoa mikopo kwa wastaafu kupitia mfuko wa pensheni wa PSPF kwa kushirikiana na Benki ya Posta Tanzania TPB.

Mpango huo ambao unajulikana kama 'Wastaafu Loan' umelenga kukidhi mahitaji halisi ya fedha kwa wastaafu kwa mikopo ya gharama za matibabu, ada za shule, kuendesha biashara na miradi mbali mbali.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa huduma hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa PSPF, Adamu Mayingu amesema utafiti waliofanya unaonesha kuwa wastaafu wanaingiza kiasi kikubwa cha fedha katika uchumi kutokana na mafao wanayolipwa ambayo kama watawekewa mfumo mzuri wanaweza kuleta athari chanya za uchumi.

Naye Mkurugenzi wa Benki ya Posta Sabasaba Moshingi amesema mkopo huo ambao ni wa kwanza katika soko la Benki utawasaidia wastaafu kwani hauna dhamana na kuongeza kuwa mkopaji anaweza kukopa kuanzia shilingi 500,000 hadi milioni 20 kwa riba ndogo ya asilimia 12, zitakazolipwa kupitia pensheni yake ya mwezi ndani ya mwaka mmoja hadi mitatu.