Wednesday , 16th Mar , 2016

Imebainika kuwa vitendo vya rushwa, matusi kwa baadhi ya watumishi wa afya kwenye baadhi ya vituo vya afya na zahanati jijini Mwanza ndio chanzo cha wanawake wajawazito kutohudhuria kiliniki na kujifungulia nyumbani.

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Manju Msambya

Taarifa hiyo imetolewa na shirika la Tandabui linalojihusisha na afya ya Uzazi wakati wa uwasilishaji wa taarifa za ufatiliaji wa kamati iliyoundwa kwa lengo za kuhakikisha jamii inafikiwa na huduma bora za afya sambamba na kujua haki zao.

Katika taarifa ya shirika hilo imesema kuwa rushwa na lugha chafu kwa kina mama hao ndio sababu ya wengi wao kujifungulia nyumbani hali ambayo inasababisha vifo vya kina mama na watoto kuongezeka katika wilaya hizo.

Kamati hiyo imesema imebaini kuwa pia kulikua na wizi wa dawa za kinamama hao wajawazito kitu ambacho kilikua kinasababisha ukosefu wa dawa katika baadhi ya vituo hali iliyopelekea kina mama wengi kukosa huduma muhimu wakati wa kujifungua.

Baada ya Taarifa hiyo Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilemela Nyagini Vinias amesema endapo mtumishi yoyote atabainika anaendelea kutoa kauli zisizostahili katika utoaji huduma basi hatua za kisheria zitashukuliwa dhidi yake.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Manju Msambya ametua fursa hiyo kuwataka watumishi ambao wamepewa dhamana ya kuwahudumia wananchi waifanye kwa weledi ikiwa ni pamoja na kuwajali wananchi wanaokwenda kupata huduma hiyo.