Tuesday , 10th Jun , 2014

Ofisi ya Taifa ya Takwimu nchini Tanzania leo imetoa chapisho kuu na la tatu la Sensa ya watu na makazi huku likionyesha kuwa idadi ya watu nchini imeongezeka kutoka watu milioni 44 na laki tisa hadi milioni 48 kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete.

Akizindua chapisho hilo jijini Dar es Salaam leo, Rais Jakaya Kikwete amesema ongezeko hilo la idadi ya watu linatokana na kasi ya ukuaji wa idadi ya watu ambayo kwa sasa kuna ongezeko la asilimia 2.7 huku akizitaka ofisi na taasisi za umma kutumia takwimu hizo kwa ajili ya kupanga miradi ya maendeleo pamoja na kupunguza kiwango cha umasikini.

Awali akitoa taarifa za msingi zilizomo ndani ya chapisho hilo, Mkurugenzi Mkuu wa ofisi ya taifa ya takwimu Dkt. Albina Chuwa amesema theluthi moja ya kaya zote nchini zinaongozwa na wanawake, ambapo amekitaja chanzo cha hali hiyo kuwa ni kutokana na umaskini unaozikabili kaya nyingi nchini.