Tuesday , 24th May , 2016

Serikali imesema uamuzi wa kuanzisha eneo huru la Kiuchumi (EPZ), katika mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani mkoani Manyara unalenga kudhibiti utoroshwaji wa madini ya Tanzanite.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage.

Akijibu swali la Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya (CHADEMA), Waziri wa Viwanda ,Biashara na Uwekezaji, Mhe Charles Mwijage, amesema hadi sasa serikali inahitaji hekta 1,500 ili kukamilisha mradi huo.

Mwijage amesema serikali tayari imeshaanza mazungumzo na wawekezaji mbalimbali na hivyo mradi huo utaanza mara moja ili kudhibiti utoroshaji huo wa madini.

Waziri Mwijage amesema Mkoa wa Manyara umeshatenga hekta 530 kwa matumizi ya kujenga mradi huo lakini serikali inaomba eneo hilo liongezwe hadi kufikia hekta 1,500.

Amesema eneo lilitengwa lipo katika kijiji cha Kandasikra, wilayani Simanjiro ambapo juhudi za kutenga eneo hilo zilianza mwaka 2007 lakini taratibu hizo zilikamilika Julai mwaka jana.

Waziri huyo amesema kuwa ucheleweshwaji huo ulitokana na ulipaji wa fidia kwa wakazi sita ambao hawakuwa wamefanyiwa tathmini waliokuwa wakidai shilingi milioni 15.