Tuesday , 10th Mar , 2015

Shule ya sekondari idodi iliyopo tarafa ya idodi wilaya ya Iringa vijijini imelazimika kufungwa kwa wiki mbili kufuatia kutokea kwa ajali ya moto kwenye bweni la wasichana ili kupisha uchunguzi wa chanzo cha moto huo pamoja na ukarabati wa majengo.

Mkuu wa wilaya ya iringa Angelina Mabula.

Mkuu wa wilaya ya Iringa Angelina Mabula ameyasema hayo wakati akizungumza na wazazi wa wanafunzi wa shule hiyo, wananchi pamoja na wanafunzi.

Akizungumzia tukio hilo mkuu wa shule hiyo Christopher Msomola amesema tukio hilo limetokea majira ya saa tisa mchana ambapo ndani ya bweni hilo kulikuwa na mwanafunzi mmoja aliyekuwa akiumwa na wengine wachache ambao ndio waliotoa taarifa ya kutokea kwa moto huo.

Amesema kuwa hakuna mwanafunzi aliyejeruhiwa lakini wanafunzi 14 walipoteza fahamu kutokana na mshituko na vyumba vinne viliteketea na vingine wananchi walifanikiwa kuokoa mali za wanafunzi.

Hata hivyo kwa upande wao wanafunzi wakizungumzia tukio hilo wamesema kuwa ajali hiyo ya moto inawaathiri kimasomo na kuhofia kufeli kutokana na kuwa wanapoteza vitendea kazi vya shule pamoja na kuwa na hofu juu ya usalama wao wanapokuwa ndani ya bweni.

Bweni hilo la wasichana la Benjamini William mkapa ni mara ya tatu kuungua moto ambapo mwaka 2009 ajali hiyo ilisababisha vifo vya wanafunzi na ndani ya mwaka huu ajali hiyo imetokea mara tatu hali iliyopelekea wazazi na wakazi wa eneo hilo kuhisi kuwa inachangiwa na imani za kishirikina.