Monday , 1st Dec , 2014

Mbunge wa Nzega Dkt Hamis Kigwangalla amekemea tabia ya serikali kutochukua hatua kali za kisheria kwa baadhi ya viongozi wanaochukua mali za umma na kugawana kama karanga inawafanya wananchi kukosa imani ya serikali yao kuwa na  hasira.

Mbunge wa Nzega Dkt Hamis Kigwangalla

Tabia ya serikali kutochukua hatua kali za kisheria kwa baadhi ya viongozi wanaochukua mali za umma na kugawana kama karanga inawafanya wananchi kukosa imani ya serikali yao kuwa na  hasira na pengine  kusababisha kutoweka kwa amani kwa kuwa hakuna mtu anayeweza kuvumilia shida wakati anaona watu wachache wakigawana mali ya umma na kuendelea na nyadhifa zao.

Mwenyekiti wa kamati ya bunge ya TAMISEMI Dk. Hamisi Kigwangalla ametoa kauli hiyo katika ibada iliyofanyika katika kanisa la KKKT usharika wa Mara mkoani Arusha iliyoambatana na uzinduzi wa albam ya kwaya inayowasihi viongozi kuwa waadilifu na kuongeza kuwa  viongozi waliopewa dhamana ya kuliongoza taifa wasipo tekeleza wajibu wao ipasavyo na kujiingiza katika ufisadi huku wakiangaliwa kama watakatifu  inaweza kuondoa amani ya nchi hii. 

Aidha Dk. Kigwangalla ameongeza kuwa ni jambo la kushangaza kuona watu wachache wanapewa nafasi ya kukaa muda mrefu katika madaraka huku wakiendelea kufuja fedha za umma wakati kuna watu wengi vijana wenye uwezo wa kuongoza na kamwe watanzania wa sasa hawatakuwa tayari kuendelea kuona wezi wakifukuzwa kazi bila kuchukuliwa hatua ikiwemo kufungwa na kufilisiwa mali zao ili kukomesha tabia za ufisadi kwenye rasilimali za taifa.

Kwa upande wake mchungaji kiongozi wa kanisa la KKKT usharika wa mara Diyosisi ya Kaskazini kati mchungaji Herbert Mkemwa amesema matukio hayo yanatokana na binadamu kutomwogopa Mungu na wengine wamejificha katika vivuli vya dini lakini siyo wema na hata hivyo utandawazi umechangia kuondoa uadilifu kwa watanzania huku kaimu mkuu wa mkoa wa Arusha Nyirembe Mnasa akiainisha namna ya kupata kiongozi Mwadilifu.