Friday , 30th Sep , 2016

Licha ya kuimarika kwa hali ya usalama, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR nchini Burundi limekiri kuwa idadi ya wakimbizi wanaosaka hifadhi nje ya taifa hilo imeongezeka.

Wakimbizi wa Burundi wakiingia Tanzania

Lakini shirika hilo limesema kuwa idadi hiyo inajumuisha wakimbizi waliokuwepo katika nchi za awali.

Mwakilishi mkazi wa UNHCR nchini humo Abel Mbilinyi amefafanua kuwa idadi iliyotolewa mapema wiki hii na UNHCR ya laki tatu inatokana na ukweli kwamba kila aliyekimbia nchini humo mwaka jana kutokana na hali ya kisiasa, ni mkimbizi.

Abel Mbilinyi amesema kuwa wakimbizi waliorudi katika vuguvugu la kisiasa nchini humo wanahesabiwa kuwa ni wakimbizi lakini Umoja wa Mataifa unawatambua wakimbizi wale tu walioomba vibali vya ukimbizi katika nchi tofauti.

Mbilinyi amesema UNHCR ilikuwa na mkutano mapema wiki hii jijini Nairobi, Kenya kujadili hali ya wakimbizi na wahamiaji katika ukanda wa maziwa makuu.