Tuesday , 9th Sep , 2014

Serikali ya Tanzania imetakiwa kuitisha uchaguzi wa serikali za mitaa, ambao hufanyika kila baada ya mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu, pamoja na utekelezaji wa shughuli za uboreshaji wa daftari la wapiga kura.

Katibu Mkuu wa Chadema Dkt Wilbrod Slaa.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam jana na katibu mkuu mpya wa baraza la wazee CHADEMA taifa Bw. Rodrick Lutembeka ambapo amehoji kuwa tume ya uchaguzi iliahidi kuwa mwezi septemba watatoa ratiba ya uandikishwaji wa wapiga kura lakini mpaka sasa ipo kimya kuhusiana na suala hilo.

Awali CHADEMA kupitia Mkurugenzi wa Operesheni na Mafunzo, Benson Kigaila alitangaza matokeo ya uchaguzi wa baraza la wazee taifa ambao wamechaguliwa kupitia uchaguzi wa ndani ukishikirisha wawakilishi wa wazee 90 kutoka mikoa ya Tanzania bara na Zanzibar.

Wakati huo huo, wilaya ya Karatu jijini Arusha ni miongoni mwa wilaya zinazokabiliwa na changamoto ya mimba za utotoni mashuleni hali ambayo wadau wa elimu wanasema jitihada za makusudi zinahitajika zikiwemo kujenga hosteli katika shule za kata ambazo ndizo zinazoathirika zaidi na tatizo hilo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa jengo la utawala katika shule ya Dkt. Wibroad Slaa, Mwalimu mkuu wa shule hiyo Bi. Farida Silayo amesema hali hiyo inatokana na wanafunzi wengi wa kike kulazimika kuishi kwenye nyumba za kupanga bila usimamizi.

Silayo ameongeza kuwa wanafunzi wa kike wanaopata ujauzito wakiwa mashuleni wilayani humo wamekuwa wakishindwa kupata haki zao za msingi ikiwa ni pamoja na kuwajibishwa watuhumiwa wanowapa ujauzito na hii ni kutokana na halmashauri kutetenga fungu kwa ajili ya kuwasaidia watoto wa kike.