Jumanne , 15th Oct , 2024

Jumuiya ya nchi za kusini mwa Afrika zimeandaa mpango mkakati wa kumaliza changamoto za umeme zilizokuwa zinawakabili na kusababisha kupunguza uzalishaji katika nchi 12 kwa kusaidiana umeme kutoka nchi moja kwenda nyingine.

Hayo yamesemwa na Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Khatibu Kazungu kwenye kongamano la nchi za kusini mwa jangwa la Sahara lililolenga kutatua changamoto za umeme miongoni mwa nchi hizo.
“Ni kwa namna gani tunaweza tukatumia vyanzo vyetu Vya umeme kwa pamoja kwa kushirikiana katika nchi hizi wanachama wa SADC, katika kufua umeme, kusafirisha na katika kusambaza umeme kwa wateja, sisi Kama Serikali Tuna mradi unaitwa TAZA, mradi uliokusudia kuunganisha miundombinu Kati ya Tanzania pamoja na Zambia na wakati mwingine tunapokutana kwenye vikao Kama hivi kupitia mikakati hiyo na hatua tulizofikia so far changamoto ambazo tunakutana nazo na namna gani tujipange vizuri ili kuweza kutatua changamoto hizo”, Khatibu Kazungu-Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati.

Aidha Tanesco wanaelezea namna wanavyonufaika na umoja huo.
“Sisi Kama Tanesco Kama nchi, tupo katikati ya Pools mbili upande wetu wa Kaskazini na Kusini, tuna miradi ambayo inatuunganisha na Kenya kwa maana tukishajiunga na Kenya kwa maana tumejiunga na East African power pool na Southern Africa Power Pool, hii inatupa uwezekano wa power exchange kwa maana ya mauziano ya umeme katika nchi hizi kutoka nchi moja kwenda nyingine hii maana yake nchi moja wapo inapokuwa na shida nchi nyingine inachukua jukumu la kumsaidia”,  Mhandisi Costa Bagumya-Naibu Mkurugenzi Mtendaji Tanesco.

Nao baadhi ya wananchi wanaelezea faida za umeme wa uhakika kwenye shughuli za kiuchumi.
“Sasa hivi umeme wa uhakika tunaendesha biashara zetu fresh Kama Mimi nipo mgahawani kwahiyo tunapoza vinywaji vyetu, tunaweka vyakula kwenye friji na biashara zetu zinaenda vizuri sana”,  Suleiman Kalumanzira -Mkazi wa Dar es Salaam
“Umeme wa uhakika unatusaidia kwenye shughuli za uzalishaji Kama viwanda ajira zinaongezeka kwa maana umeme wa uhakika upo na unatuzalishia vitu mbalimbali”, Henry Temba-Mkazi wa Dar es Salaam.

Aidha nchi ya Tanzania kwa sasa kupitia mradi wa kufua umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere unazalisha takribani megawat 700 na ndani ya muda mchache utaanza kuzalisha megawat 900, lakini kupitia chanzo cha nishati ya jua kinazalisha megawat 600, kutumia joto ardhi inazalisha megawat 5000 na mikakati iliyopo ni kuanza kuuza umeme huo kwa nchi nyingine.