Jumanne , 1st Oct , 2024

Serikali imesema inatarajia matokeo chanya mara baada ya uwekezaji wa takribani Trilioni 40 uliofanywa kwenye miundombinu ya Bandari, Meli, viwanja vya ndege na ununuzi wa Ndege.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mkakati wa upakiaji wa mizigo ili kuimairisha biashara ya usafirishaji wilayani Kilosa kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Doto Biteko Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile amesema malengo makubwa ya uwekezaji huo ni pamoja na kuzitengenezea mazingira mazuri ya kujiendesha bila ruzuku.

"Serikali inawezekeza fedha zote hizi kwa malengo ya kuhakikisha taasisi zinajitegemea na kujisimamia bila kutegemea ruzuku kutoka serikali kuu,hivyo mkakati huu tunategemea utaleta mageuzi katika sekta ya uchukuzi”

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Prof. Godius Kahyarara amesema mkakati huo umewahusisha wadau wote ili kuhakikisha unakuwa endelevu na wenye tija.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania(TRC) Masanja Kadogosa amesema mabehewa nane ambayo yamefadhiliwa na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa utekelezaji wa mpango huo yatawezesha bidhaa za nyama na mbogamboga kuwahi kwa walaji kwa wakati.