Jumanne , 17th Sep , 2024

Mtoto Rwegasila Jackson (14) mkazi wa wilaya ya Muleba mkoani Kagera anahofiwa kufa maji baada ya kuzama ndani ya Ziwa Victoria wakati akiogelea na wenzake kwenye fukwe za Gymkana Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.

Akizungumza na EATV Agripina Wiston Mkazi wa Buyekela ambaye ni dada mlezi wa mtoto huyo aliyemtoa kijijini kwa ajili ya kumfanyia kazi ya kutembeza vyombo (machinga) amesema kuwa siku ya Jumapili alimuaga anaenda kudai fedha kwa wateja wake.

"Siku ya Jumapili hatukufanya kazi ilivyofika jioni mida ya saa tisa akaniambia jioni naomba niende kuzurura kidogo halafu pia kuna mtu ninamdai niko na rafiki yangu, baadae nilipoenda na mimi kutembea ufukwe wa Gymkana nikamkuta kijana aliyetoka naye anavaa nguo nikashtuka kwanza kumuona akaniambia ulivyoturuhusu sisi tumekuja huku kuogelea nikamwambia fanya haraka umuite Rwegasila tuondoke akaniambia hamna Rwega maji yamemchukua,"" Amesema Agripina.

Afisa Habari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoa wa Kagera Shaban Mussa amesema jitihada zinaendelea za kuhakikisha mwili wa Rwegasila unaopolewa.