Jumatano , 4th Feb , 2015

Chama cha Baseball nchini TABSA kimesema hivi sasa kipo katika mpango wa kuendeleza na kuanzisha vipya katika mikoa mbalimbali hapa nchini ili kuweza kuwa na wachezaji wengi na wenye kuweza kuitangaza nchi katika mchezo huo.

Akizungumza na East Africa Radio, Katibu Mkuu wa TABSA, Alpherio Nchimbi amesema, mpaka sasa wameanza mkakati wa kuongeza vilabu kwa jijini Dar es salaam katika wilaya za Ilala, Temeke na Kinondoni huku Mkoa wa Mbeya na mikoa ambayo itakuwa tayari kuwa na vilabu kupelekewa walimu kwa ajili ya kukuza mchezo huo hapa nchini.

Nchimbi amesema, licha ya kuongeza vilabu pia wamekiomba chama cha Baseball Afrika AFAB ili kuweza kupatiwa kozi ya walimu wa mchezo huo katika shule 12 hapa nchini ambapo katika kila shule atatoka mwalimu mmoja kwa ajili ya kuhudhuria kozi hiyo.

Nchimbi amesema programu hiyo pia itasaidia kwa kiasi kikubwa katika kupata walimu wengi wa mchezo huo kwani baada ya kumaliza na walimu hao 12 wanatarajia kuwa na kozi mbalimbali zikiwa na lengo la kupata walimu watakaoweza kufundisha katika vilabu mbalimbali hapa nchini.