Jumanne , 10th Mei , 2022

Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana, amesema licha ya kwamba Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) inafanya jitihada kubwa ya kuhamasisha utalii lakini bado jitihada hizo haziendani na utajiri mkubwa wa mazao ya utalii yaliyopo Tanzania na hivyo kuwataka waongeze ubunifu.

Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana

Waziri Dkt. Chana, ametoa wito huo alipokutana na menejimenti ya Bodi hiyo na kuwataka wahakikishe wanabuni programu mbalimbali za kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini Tanzania.

Waziri Chana ameongeza kuwa, ipo haja kwa Bodi hiyo kuongeza nguvu kwa ajili ya kuelimisha umma juu ya umuhimu wao kushiriki kikamilifu katika masuala ya Utalii.

Akielezea Mafanikio mbalimbali yaliyotokana na utendaji wa Bodi hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Bodi hiyo Felix John, ameyataja kuwa ni pamoja na kuongeza masoko katika nchi mbalimbali kama China, Urusi, India, nchi za Kiarabu na Ulaya.