Jumatano , 10th Mei , 2017

Watu watano wa familia moja katika kijiji cha Ng'iresi Kata ya Sokoni Two Wilayani Arumeru Mkoani Arusha wamefariki baada ya nyumba yao kuangukiwa na mti wa Mkuyu usiku wa kuamkia jana kufuatia mvua kubwa zinazoendelea kunyesha Mkoani huko.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo, amesema mti huo wa Mkuyu uling'olewa na upepo kutoka kwenye mlima Lakimana ambao wananchi wengi wamejenga chini ya mlima huo kutokana na uhaba wa ardhi.

Kamanda Mkumbo amewataja waliofariki katika tukio hilo kuwa ni mtoto mkubwa wa kiume wa familia hiyo Gilliad Jonathan, Glory Jonathan, na Miriam Balozi ambao ni wanafunzi Cuthbert Jonathan na Lazaro Lomunyaki

Kamanda huyo amewataja walionusurika kwenye tukio hilo ambao walikuwa pia ndani ya nyumba kuwa ni Zakayo Jonathan na Josephat Jonathan.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, Dk Wilson Mahera amewataka wananchi kutohusisha tukio hilo na imani za kishirikina baada ya kusikika taarifa za uchawi kuhusiana na kuanguka kwa mti huo.