Alhamisi , 17th Nov , 2016

Mtuhumiwa wa kufadhili vitendo vya ugaidi Azan Abubakar (23) amefikishwa mahakamani leo na kusomewa mashtaka mawili ya kutuma fedha kwa njia ya simu zilizokuwa na ujumbe wa kufadhili vitendo hivyo.

Sheria na haki

 

Abubakar amefikishwa mahakamani mbele ya hakimu mfawidhi wa Wilaya ya Dodoma, Mwajuma Lukindo ambapo alisomewa mashtaka mawili ya kutuma fedha kwa ajili ya kufadhili vitendo vya ugaidi na mawakili wawili wa serikali, Costantine Kakula na Kezilahabi Miyango.

Kakula alidai mbele ya hakimu kuwa mnamo Mei 15 mwaka huu mkoani Dodoma mahali pasipojulikana mtuhumiwa alituma kiasi cha fedha sh. 265,000 iliyokuwa na ujumbe wa kufadhili vitendo vya ugaidi kwenda kwenye namba ya simu +254708104109 yenye jina la Mohamed Ibrahim.

Katika shtaka la pili ilidaiwa kuwa mnamo Julai 22 mwaka huu mtuhumiwa alituma kiasi cha fedha sh. 148,000 kwenda kwenye namba hiyo hiyo ya Mohamed Ibrahim iliyokuwa na ujumbe wa kufadhili vitendo vya ugaidi.

Hata hivyo mtuhumiwa hakutakiwa kujibu kitu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi za ugaidi ambapo upande wa serikali ulisema kuwa upepelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Mtuhumiwa amerudishwa rumande hadi Desemba Mosi mwaka huu kesi yake itakapotajwa tena.