Jumatano , 9th Nov , 2016

Waliokuwa viongozi katika Shirikisho la Soka nchini tanzania (TFF), Martine Chacha na Juma Matandiko wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Jijini Dar es Salaam na kusomewa mashitaka ya kuomba rushwa.

Jamal Malinzi - Rais wa TFF

 

Viongozi hao wanatuhumiwa kuomba rushwa ya shilingi milioni 25 kutoka Geita Gold Sports ili kuisaidia iweze kupanda daraja, kutoka Ligi Daraja la Kwanza hadi Ligi Kuu Tanzania Bara, mwishoni mwa msimu uliopita.

Watuhumiwa hao ambao mmoja wapo (Juma Matandiko) alikuwa ni msaidizi wa Rais wa TFF, alijiuzulu nafasi yake, mara baada ya kuvuja kwa sauti inayodaiwa kumuhusisha pia yeye, ambayo ilikuwa ikipanga njama ya kuisaidia timu ya Geita Gold ipande daraja kwa kuikandamiza timu ya Polisi Tabora ambayo ndiyo ilikuwa na upinzani na Geita.

Wote wamekana mashitaka, na kesi hiyo itatajwa tena Novemba 30 mwaka huu.

Geita Gold Sports

Sakata hilo la kupanga matokeo ndilo liliilazimu TFF kuzishusha daraja timu nne zikiwemo Geita Gold na Polisi Tabora zilizoshushwa hadi Ligi daraja la Pili na kufanya maamuzi ya kuipandisha daraja timu ya Mbao FC, ambayo hadi sasa inashiriki Ligi Kuu Tanzania Bara.