Ijumaa , 10th Jul , 2015

Idadi ndogo ya wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi nchini Tanzania kimesababisha kupunguza ugunduzi katika nyanja mbalimbali kitu ambacho kinarudisha maendeleo yanayotokana na sayansi na teknolojia.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkurungenzi wa Taasisi inayosimamia ugunduzi kwa wanafunzi (YST), Dkt. Gosbert Kamugisha ambapo amesema idadi hiyo kudhoofisha maendeleo hasa katika masuala ya utafiti utakaosaidia jamii kuondokana na matatizo yanayowakabili.

Dkt Kamugisha amesema mbali na kuwepo kwa jitihada za kuhakikisha wanafunzi wengi wanasoma masomo ya sayansi lakini kumekuwepo na mafunzo kidogo kwa vitendo kutokana na maabara zilizopo kukosa vifaa muhimu kwaajili ya kujifunza na kufanya utafiti.

Ameongeza kwa kutambua jitihada za wanafunzi wa sayansi wanaofanya utafiti na wabunifu takribani wanafunzi 60 watazawadiwa zawadi mbalimbali ikiwemo pesa taslim, medali, vikombe, vifaa vya maabara na wanafunzi sita watazawadiwa udhamini wa kusoma vyuo vikuu kusoma shahada za sayansi na teknolojia.

Kwa upande wake mwakilishi kutoka ubalozi wa Ireland Bw. Brian Nolan amesema mashindano hayo yanajumuisha wanafunzi 240 na walimu 120 kutoka mikoa yote ya Tanzania na Zanzibari na yataanza kuanzia tarehe 6-7 mwezi August 2015.