Alhamisi , 25th Jun , 2015

Serikali imetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo walimu wa sekondari nchini wanaofundisha masomo ya jiografia, hesabu, Kiswahili na kiingereza katika shule mbalimbali za serikali nchini.

Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia akifafanua jambo.

Akifungua mafunzo hayo jana kwenye ukumbi wa shule ya sekondari ya Dodoma, Waziri wa TAMISEMI, Hawa Ghasia amewataka walimu hao kuwa chachu ya ufaulu wa wanafunzi hasa wale walioko kidato cha nne.

Amesema mafunzo hayo ni mojawapo ya mikakati ya serikali katika kufanikisha matokeo makubwa sasa (BRN) ambapo serikali imejiwekea wastani wa ufaulu kwa wanafunzi kufika asilimia 80 ya ufaulu kwenye mitihani ya kitaifa kwa mwaka 2015.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa walimu wanaopata mafunzo hayo kutoka katika wilaya za Chemba, Kondoa na manispaa ya Dodoma mkoani hapa, Abdallah Mrisho alisema kuwa mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka kwani yatasaidia kuinua kiwango cha elimu nchini kwa faida ya vizazi vijavyo.