Jumamosi , 16th Dec , 2017

Mbunge wa Kigoma mjini Mh. Zitto Kabwe ambaye ni mdau mkubwa wa michezo hususani soka amekiombea aunacham wa FIFA chama cha soka cha Zanzibar ZFA.

Hatua hiyo imekuja baaada ya timu ya taifa ya Zanzibar (Zanzibar Heroes) kutinga hatua ya fainali ya michuano ya CECAFA Senior Challenge 2017 inayoendelea nchini Kenya.

Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Facebook Zitto amefunguka ya moyoni akitaka ZFA iwe mwanachama wa shirikisho la soka la kimataifa FIFA pamoja na lile la Africa CAF angalau kwa miaka mitano na inaweza kupiga hatua ambazo TFF imeshindwa.

“Kama hatutaki Zanzibar kuwa Mwanachama wa FIFA kama ilivyo Scotland. Tuseme kwa miaka 5 ijayo kuanzia mwaka huu ZFA ndio mwanachama FIFA na CAF ili TFF ipate muda wa kujipanga. Ndani ya hiyo miaka 5 nawaambia Zanzibar itakwenda AFCON na hata Kombe la Dunia. #MsemaKweliMpenziWaMungu”, ameandika Zitto Kabwe.

Zitto ametoa mfano kuwa Zanzibar ingepata uanachama kamili wa FIFA kama ilivyo kwa nchi za Scotland pamoja na Wales ambazo pia ni nchi dada za taifa la Uingereza lakini zinatambuliwa na FIFA kama mataifa wanachama huku Uingereza ikitambulika kama England.