
Wawakilishi pekee wa Tanzania kwenye michuano ya kimataifa ya vilabu barani Africa Yanga SC tayari imewasili mjini Antalya, Uturuki kwa kambi ya siku tano kujiandaa na mchezo wake wa pili wa Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya TP Mazembe ya DRC, June 28 mwaka huu, Dar es Salaam.
Yanga imefikia sehemu, ambako pia waliweka kambi kabla ya mchezo wao wa kwanza wa kundi hilo dhidi ya Mouloudia Olympique Bejaia.
Ikumbukwe Yanga SC ilianza vibaya mechi za Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika, baada ya kufungwa bao 1-0 na wenyeji Mouloudia Olympique Bejaia, kwenye uwanja wa Unite Maghrebine mjini Bejaia Jumapili iliyopita, huku wapinzani wao TP Mazembe wenyewe wakianza kwa ushindi wa 3-1 dhidi ya Medeama ya Ghana mjini Lubumbashi.
Yanga itakuwa na wakati mgumu kwa mchezo huo dhidi ya TP Mazembe ikiwa bado wiki mbili mbele, kwa sababu ya kukosa huduma ya walinzi wake Nadil Haroub anayecheza kati, na mlinzi wa kushoto, Haji Mwinyi wenye kadi za kukosa mechi mbili kila mmoja, huku Oscar Joshua anayecheza kushoto pia na Juma Abdul anayecheza kulia wakiwa ni majeruhi.