Alhamisi , 22nd Aug , 2024

Rais wa Tanzania Dokta Samia Suluhu ametoa rai kwa wadau wa maendeleo nchini kuzidi kuwekeza kwenye sekta ya michezo nchini ili kuendeleza vipaji vya wanamichezo na kuzidi kuitengenezea sifa ya nchi kwenye medani za kimataifa

Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa Jiwe la Msingi kwenye kituo cha Suluhu Sports Academy  kilichopo kwenye eneo la Kizimkazi mjini Unguja-Zanzibar leo Agosti 22-2024, Rais Samia amesema Serikali inatambua idadi kubwa ya vijana nchini na Serikali inafanya jitihada zaidi kutengeneza miundombinu ya michezo ili kuendeleza sekta ya michezo hapa nchini.

“Kama tunavyofahamu kuwa asilimia kubwa ya Watanzania ni Vijana ,hivyo basi Serikali kupitia Nyanja mbalimbali tunajenga miradi kadhaa ya vijana ,Mradi huu wa Suluhu Academy unabeba taswira pana na ndoto kubwa kwa vijana wa sasa na wajao kwa ajili ya wachezaji wenye vipaji” amesema Rais wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan

Kwa upande mwingine,Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa  ametoa pongezi kwa Rais Samia kwa kuweka mfumo mzuri wa maendeleo ya michezo kwa kuongeza ushindani  ndani ya ligi zetu za ndani na kuleta ushindani kimataifa na kuiletea sifa Tanzania kwenye medani ya soka.

Ujenzi wa Suluhu Sports Academy unataraji kukamilika mnamo Aprili 2025 huku itahusisha uwanja wa kuchezea mpira wa miguu ambapo itachukua watazamaji elfu 20,000 huku itahusisha michezo mingine changamani kwenye eneo hilo la Mkunguni,Zanzibar