Ijumaa , 15th Dec , 2017

Wachezaji wa Yanga mshambuliaji Amisi Tambwe pamoja na kiungo Thabani Kamusoko ambao walikuwa majeruhi wa muda mrefu, wamerejea kikosini ambapo wanafanya mazoezi mepesi kwaajili ya kurejesha makali yao.

Afisa habari wa klabu hiyo Dismas Ten amesema klabu hiyo inaendelea na maandalizi ya michuano mbalinbali inayoikabili ikiwemo klabu bingwa ya Afrika ambayo wamepangwa kuanza na klabu ya St. Louis ya Shelisheli.

“Taarifa nzuri ni kwamba Kamusoko na Tambwe wameanza kufanya mazoezi, Tambwe anafanya mazoezi kwa asilimia mia moja na Kamusoko anaendelea na mazoezi mepesi ili kuweza kurejea kwenye ubora wake”, amesema Ten.

Ten ameongeza kuwa timu ina majeruhi mmoja, mlinzi wa kati Kelvin Yondani ambaye aliumia kwenye majukumu ya timu ya taifa ya Tanzania bara (Kilimanjaro Stars) iliyokuwa inashiriki michuano ya CECAFA na iliondolewa katika hatua ya makundi.

“Tuna majeruhi, Yondani ambaye aliumia akiwa na timu ya taifa na tayari daktari ameshathibitisha kuwa atakuwa nje hadi Desemba 28 ambapo ataanza mazoezi kwaajili ya kurejea uwanjani”, amemaliza Ten.