Jumanne , 9th Dec , 2014

Timu ya Taifa ya mchezo wa Kriketi ya wanawake inatarajiwa kuelekea Afrika Kusini Desemba 12 mwaka huu kujiandaa na michuano ya kufuzu kushiriki michuano ya Kombe la Dunia inayotarajiwa kufanyika nchini humo Desemba 13 mwaka huu.

Akizungumza na East Africa Radio, Mtendaji mkuu wa Chama cha mchezo wa Kriketi nchi TCA, Zurri Remtullah amesema maandalizi yamekamilika kwa ajili ya michuano hiyo ambapo kuna baadhi ya wachezaji walio katika kikosi cha vijana chini ya umri wa miaka 19 watakaojiunga na kikosi cha timu ya Taifa kwa ajili ya kuboresha timu hiyo.

Remtullah amesema anaamini timu hiyo itafanya vizuri kutokana na maandalizi mazuri yaliyofanyika ikiwemo kuwaandaa vizuri vijana ili kuweza kufanya vizuri pindi watakapoungana na kikosi cha timu ya Taifa.

Zurri amesema timu ya Taifa imekwishacheza baadhi ya mechi za kirafiki na timu mbalimbali ikiwa ni sehemu ya kujihakikishia inajiweka katika nafasi nzuri katika michuano hiyo.