Jumapili , 9th Jul , 2017

Uongozi wa klabu ya Yanga umewatoa hofu mashabiki wa timu hiyo juu ya wachezaji waliomaliza mikataba yao na kudai kila mchezaji wanayemhitaji atabaki katika timu hiyo kwa kumpa mkataba mpya.

Deus Kaseke

Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Boniface Mkwasa, amesema ripoti ya kocha wao, George Lwandamina, imeeleza wazi wachezaji ambao anataka wabaki kwenye timu hiyo na uongozi utafanya jitihada zote kuwabakiza.

Kauli hiyo ya Mkwasa imekuja siku chache baada ya taarifa kuzagaa kuwa kiungo wao, Deus Kaseke, yupo mbioni kusajiliwa na klabu ya Singida United baada ya kumaliza mkataba wake na Yanga.

Hata hivyo, inafahamika kuwa uongozi wa Yanga umeshtukia dili hilo na kuamua kumrejesha Kaseke Dar es Salaam kutoka Mbeya kwa ajili ya kumsainisha mkataba mpya.

Kaseke alishaanza mazungumzo na Singida United na walikuwa kwenye hatua za mwisho kumalizana ili msimu ujao aichezee timu hiyo.