Alhamisi , 31st Mar , 2022

Baada ya mataifa manne kati ya matano yatakayoiwakilisha africa katika kombe la dunia nchini Qatar baadae mwezi November mwaka huu kufanya vizuri wakiwa na makocha wazawa wa nchi zao, inaonekana imani imeanza kuongezeka kwa nchi za Africa katika kuwaamini makocha wenye asili ya nchi zao.

( Habib Kolo Toure )

Hali hiyo imekuja baada ya kuwepo kwa taarifa kutoka jiji la Abidjan nchini Ivory Coast zinazodai kuwa kocha Patrice Baumelle anayeinoa timu ya taifa ya nchi hiyo kwasasa hataongezewa tena mkataba, na badala yake chama cha soka nchini humo kikiwa tayari kuanza mazungumzo na Gwiji Habib Kolo Toure ili kuchukua mikoba ya kuifundisha Taifa hilo.

Toure kwa sasa ni mmoja wa makocha wasaidizi wa kocha Brendan Rogers katika benchi la ufundi la klabu ya Leicester City inayoshiriki ligi kuu ya England. Na endapo Toure atafanikiwa kupata nafasi hiyo ya kocha mkuu wa taimu ya taifa na wakati huo huo akitaka kuendelea kuwepo katika klabu ya Leicester city anaweza kufanya kazi zote mbili kulingana na nafasi yake katika klabu hiyo.

Wawakilishi wa Africa katika kombe la dunia ni mataifa ya Ghana ‘the Black Stars’ wakiongozwa na kocha Otto Ado, Cameroon ‘the Indomitable Lion’ ikiongozwa na kocha Rigobert Song, huku Aliou Cisse akiwaongoza Simba wa Teranga Senegal na Jadel Kadri akiongoza taifa la Tunisia.