Jumanne , 23rd Jul , 2024

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini Ally Mayay Tembele ametoa wito kwa wachezaji wa zamani kutoa ushauri wa mara kwa mara kwa wachezaji wanaocheza hivi sasa juu ya somo la uzalendo na kujituma pindi wakivaa jezi ya Tanzania (Taifa Stars).

Akizungumza kwenye uzinduzi wa Taasisi ya Tanzania Veterans Sports Promotion leo Julai 23-2024,Mayay ambaye alimuwakilisha Mgeni rasmi Waziri wa Utamaduni,Sanaa na Michezo Dkt. Damas Ndumbaro amesema kumekuwa na mwenendo wa wachezaji kujituma zaidi kwenye klabu kuliko anapoichezea timu ya Tanzania Taifa Stars

“Wachezaji wastaafu tunapokutana na wachezaji wa sasa hasa wale wanaocheza timu ya Taifa kuwaeleza juu ya kujituma na kujitoa, mchezaji anaonekana kujitoa kwenye klabu yake lakini timu ya Taifa anakuwa wakawaida,” amesema Mayay

Kwa upande mwingine,Mwenyekiti  wa mashindano ya Ligi ya Veterans Tanzania Swedi Mkwabi amesema ligi hiyo itafuata uweledi na vigezo vyote huku itasaidia kuwaweka pamoja wachezaji wa zamani pamoja na kuimarisha afya zao kwa ujumla.

“Tutaenda ligi hii kwa uweledi, kuzingatia umri , malengo siku za baadae kuwapatia wachezaji wa zamani bima ya Afya wanapata matibabu halisi wakati ligi inaendelea, kuwaweka pamoja , watapata njia ya kuingiza kipato na kupata elimu ya ukocha kwa wale ambao hawajabahatika,” amesema Mkwabi.