Alhamisi , 23rd Mar , 2023

Uongozi wa klabu umeingia mkataba wa miaka miwili na Kampuni ya Masoko MobiAd Afrika ambayo inawaweka karibu wafanyabiashara kwa ajili ya kuidhamini timu yetu ya vijana wenye thamani ya Sh. 500,000,000 ambapo wanakuwa wadhamini wakuu.

Malengo ya makubaliano hayo ni kuvumbua vipaji, kuvikusanya na kuviendeleaza kwa ajili ya maendeleo ya klabu kwa siku za baadae.

Mtendaji Mkuu wa Klabu, Imani Kajula amesema kanuni ya mafanikio ya kila kitu lazima kianzie mwanzo, nasi Simba tumeona umuhimu wake tumerudi kwenye njia zetu za zamani.

Kajula amesema sio mara ya kwanza kwetu kuwa na timu za vijana ambazo zimesalisha wachezaji wengi bora ambao mpaka sasa wanatamba na timu mbalimbali za Ligi Kuu ya NBC na zile za Daraja la Kwanza.

“Sisi tunaenda mbele kwa kuleta mfumo wa kutambua vipaji, kuviweka pamoja na kuviendeleaza kutoka sehemu zote nchi nzima. Na tutaweka mfumo mzuri wazi kwa ajili ya kuwapa vijana wenye vipaji kutoka nchi nzima.

“Tunataka kuondoa bahati kwenye mpira na tunataka kuwandaa vijana wenye vipaji ili baadae kuja kuisaidia timu, na vijana watakaopatikana tutawasomesha sisi wenyewe,” amesema Kajula.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa MobAd, Rumisho Sikoni ametaja sababu ziliofanya kuingia mkataba nasi kuwa wanaamini vijana wana mchango mkubwa wa kukuza uchumi wa Taifa na mpira ni sehemu nzuri ya kupunguza tatizo la ajira nchini.

“Leo tumeingia rasmi mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya Sh. Milioni 500 kwa ajili ya kuidhamini timu ya Vijana. Lengo letu ni kukuza na kuendelea vipaji,” amesema Rumisho.

Nae Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Salim Abdallah ‘Try Again’ amesema MobiAd imekuja kipindi kizuri kwakuwa tupo kwenye mchakato wa kuanza ujenzi wa Academy yetu kwa ajili ya kukuza na kuendeleza vijana.