Ijumaa , 19th Jun , 2015

Msanii Ally Nipishe ametangaza kumuachia Mungu hatma ya mrembo aliyemwingiza katika janga hilo lililomgharimu takribam shilingi milioni 27.

Ally Nipishe

Nyota wa muziki wa Bongofleva, Ally Nipishe ambaye amerejea tena mzigoni baada ya kuvuka kiunzi cha kesi nzito ya kupatikana na gari ya wizi na kukaa jela kwa miezi 3, ametangaza kumuachia Mungu hatma ya mrembo aliyemwingiza katika janga hilo lililomgharimu takribam shilingi milioni 27 hadi kulimaliza.

Ally Nipishe amesema kuwa, kwa sasa amejikita kujenga tena misingi na kurejea katika chati na hapa kwa kifupi ameeleza kuwa, kutokana na umri wake mdogo alikata tamaa ya maisha kufuatia kesi hiyo, akiwa sasa ameamua kurejea katika muziki chini ya usimamizi wa Papaa Misifa.

Ally Nipishe amesema imemchukua takriban mwezi mzima kutuliza akili yake na kuweza kufanya ngoma mpya sambamba na video ambayo ipo tayari ikisimama kwa jina Wanapepeta Maneno.

Ally Nipishe alikutana na majanga hayo baada ya kununua gari aina ya Altezza akiunganishwa kwa wamiliki feki na aliyekuwa mpenzi wake huko Zanzibar, gari ambayo alikamatwa nayo Dar na kutiwa hatiani.