Jumatatu , 3rd Mei , 2021

Balozi wa Canada nchini Tanzania Pamela O'Donnell na Balozi wa Uingereza nchini, David Concar  leo Mei 03, 2021, wametembelea Ofisi za East Africa Television na East Africa Radio na vyombo vya IPP na kujionea shughuli mbalimbali za uendeshaji ikiwemo uandaaji wa vipindi na urushaji matanga

Wa pili kushoto Balozi wa Canada nchini Tanzania Pamela O'Donnell,na wa pili Kulia Balozi wa Uingereza nchini, David Concar wakiwa na Mkuu wa vipindi vya Radio wa East Africa, Lydia Igarabuza (Wa kwanza kulia}.

Wakizungumza mara baada ya ziara wameeleza kufurahishwa na mabadiliko ya teknolojia katika vyombo hivyo, pamoja na ufanyaji kazi katika vyombo hivyo vya habari.

Balozi wa Canada Nchini Pamela O'Donnell (wa kwanza kulia) akiwa na mtangazaji wa Kipindi cha MamaMia cha East Africa Radio Maryam Kitosi

Ikiwa leo ni siku ya  maadhimisho  ya uhuru wa vyombo vya habari duniani, mabolozi hao walipata wasaha wakuzungumza na wafanyakazi wa vyombo vya IPP Media kuhusu uhuru wa vyomBbo vya habari, huku wakigusia lengo lao la kufanya kazi na nchi nyingine katika kusaidia kuboresha uhuru wa habari.

Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, David Concar akielezewa jambo na Mkuu wa vipindi vya East Africa Radio Lydia Igarabuza

Pia wakielezea mtazamo wa vyombo vya habari nchini wamevipongeza na kuelezea kuwa vimejikita katika kuhabarisha umma huku habari zake zikijikita  kutoka mamlaka husika na zile zitokanazo na maoni ya wananchi.

Naye Mkuu wa vipindi vya Radio wa East Africa, Lydia Igarabuza akitoa hoja juu ya kipi kifanyike katika tasnia ya habari ameeleza kuwa ipo haja ya kuboresha utaalum kwa waandishi katika maeneo mbalimbali ambapo maboresho hayo yote yanaweza yakafanyika kupitia program za kuwaongezea uwezo waandishi.