Jumamosi , 30th Jul , 2016

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi nchini Tanzania Mhandisi Hamad Masauni amerejea kauli yake ya kukitaka kikosi cha jeshi la zima moto na uokoaji kuhakikisha kinafanya kazi kwa weledi

Mbali na agizo hilo, Masauni ameahidi kwamba hatavumilia uzembe wa makusudi ikiwemo kwenda eneo la tukio bila ya kuwa na vifaa vinavyotakiwa katika tukio.

Mhandisi Masauni ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam wakati alipofanya ziara katika ofisi za kikosi hicho kwa lengo la kujionea utendaji kazi wake pamoja na kufahamu changamoto zinazowakabili hasa wakati wanapotekeleza majukumu yao.

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa kikosi hicho Thobias Andengenye amesema kwa sasa tayari wameshatekeleza maagizo ya serikali ya kushirikiana kwa pamoja na jeshi la polisi ili kutumia magari maarufu kama washa-washa katika kuzima moto pale unapotokea.