Jumatatu , 5th Oct , 2020

Wenyeviti wawili wa serikali za mitaa ya Kigogo, Mbuyumi na ule wa Mwinyimkuu katika manispaa ya Ilala wamesema upanuzi wa mto Kibangu unaoendelea kwa sasa utasaidia kuondoa kero walizokuwa wanapata wananchi ya nyumba zao kuingiliwa na maji mara kwa mara hasa kwenye kipindi cha mvua.

Picha ya Mto Kibangu

Wakiongea na EATV leo wenyeviti hao Abubakari Magona, wa Kigogo Mbuyuni na Funua Ali wa mtaa wa Mwinyimkuu wamesema wananchi wamekuwa wakilazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na mto huo kujaa maji.

Wenyeviti hao wamesema kuwa kuna wakati hata usalama wa maisha ya wakazi wa maeneo yao yalikua hatarini kwa sababu nyumba nyingine zilikua kwenye kingo za mto ambao ulikua unazidi kutanuka kadri ya mvua zinaponyesha.

Tunaishukuru serikali kwa hili kwani ilikuwa ni kilio chetu cha muda mrefu cha kutaka upanuzi wa mto huu na sasa serikali imekisikia”amesema Funua Ali.

Aidha wameongeza kuwa kuna wakati watu wanakosa makazi na mahali pa kuishi kutoka na mvua hizo kuharibu kabisa makazi yao, hivyo wengi wakiishia kuwa masikini kutokana na kukosa mahali pa kuishi baada ya nyumba zao kubomolewa na maji wakati wa mvua.