Jumatano , 15th Oct , 2014

Idadi kubwa ya wamiliki na madereva wa magari hawafahamu umri wa matumizi ya matairi ya magari, kiasi kwamba wengi wao huishia kununua matairi ambayo muda wake wa kutumika umeshakwisha na hivyo kusababisha ongezeko la ajali za barabarani.

Uchunguzi wa East Africa Radio umebaini kuwa kutokana na ukosefu wa uelewa, wanunuzi wa matairi mara nyingi wamekuwa wakiangalia zaidi upya na muonekano wa matairi, badala ya alama za kitaalamu zinazoonesha tarehe ya kutengenezwa pamoja na mwaka wa ukomo wa matumizi wa matairi husika.

East Africa Radio imefanya mahojiano na mfanyabiashara wa matairi Bw. Aloyce Aron, dereva wa muda mrefu mzee Kassimu Msisi na fundi wa magari Bw. Machimu Ludovick ambao walikuwa na haya ya kusema.

Wakati huo huo, idadi ya waliokufa kutokana na tukio la ajali ya kuanguka kwa lori la mfuta huko Mbagala Rangi Tatu nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam imeongezeka na kufikia watu watano.

Akizungumza na waandishi wa habari afisa uhusiano wa hospiatli ya taifa ya Muhimbili, Bi Doris Ishinda amesema vifo vya wagonjwa wawili zaidi vimeongezeka jana jioni na usiku wa kuamkia leo na kufanya idadi ya wagonjwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili mpaka sasa kuwa kumi na moja.

Aidha katika hospitali ya Temeke wagonjwa wanne wanaendelea kupata matibabu na kufanya idadi ya wagonjwa waliolazwa mpaka sasa kupungua hadi kufikia 15 katika hospitali ya Temeke na Muhimbli na vifo imeongezeka toka vifo vitatu hadi vitano.

Kwa mujibu wa Bi. Doris Ishenda, Afisa Habari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili ambako majeruhi wa ajali hiyo wamelazwa, majeruhi watatu kati ya kumi na Tano ambao walifikishwa hospitalini hapo kufariki huku waliobakia hali zao zikiwa bado ni mbaya.

Aidha, hali ya Rais wa awamu ya pili wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar, mzee Aboud Jumbe ambaye amelazwa katika hospitali hiyo akisumbuliwa na magonjwa yanayotokana na uzee na umri mkubwa inaendelea vizuri.

Kwa mujibu wa mtoto wake wa kiume Bw. Mustafa Aboud, Rais huyo mstaafu wa Zanzibar ataendelea kuwepo hospitalini hapo kwa siku Nne zaidi ili kutoa fursa kwa madaktari kuangalia maendeleo ya afya yake.