Jumanne , 13th Feb , 2018

Waziri wa Nchi, Ofisi ya rais, Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa, Tamisemi, Seleman Jafo, amegoma kuzindua mradi wa maji katika kijiji cha Itiso wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma kutokana na baadhi ya wananchi kuharibu kwa makusudi miundombinu hiyo

Akizungumza na wananchi wa kijiji hicho, Waziri Jafo, amesema awali mkandarasi wa mradi huo alisuasua na halmashauri ya chamwino na kuamua kumbadilisha mhandisi wa maji ili kuweza kukamilika kwa haraka na kiwango bora.

Amesema wananchi wa kijiji hicho wamekuwa hawana Ushirikiano na viongozi wao na wale wa mradi hadi kusababisha kuharibu miundombinu ya maji, na kumuagiza mkurugenzi wa halmashauri ya chamwino kusimamia na wale watakaoharibu miundombinu washughulikiwe.

Naye mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Chamwino, Athumani Masasi, amesema serikali ya awamu ya tano imetoa kiasi kikubwa kwa ajili ya mradi wa maji lakini wananchi wamekuwa mstari wa mbele kuharibu miundombinu hiyo.