Jumanne , 20th Jul , 2021

Jeshi la Polisi mkoa wa Geita linawashikilia wanafunzi 11 akiwemo msichana mmoja kwa tuhuma za kuchoma moto shule ya sekondari Geita mara tatu tofauti, Julai 5, 6 na 14 huku likidai chanzo cha kufanya hivyo ni upendeleo waliokuwa wanaupata wanafunzi wanaokaa bweni.

Picha baadhi ya eneo lilioharibiwa na moto katika Shule ya Sekondari Geita (picha kutoka mtandaoni)

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Geita Henry Mwaibambe amesema uchunguzi umeonesha moto ule haukusababishwa na hitilafu ya umeme wala miundombinu chakavu ya shule hiyo, bali umefanywa na wanafunzi watukutu.

“Vinara tunaowashikilia wote ni wanafunzi, baadhi wanafunzi wa shule hii, mmoja ni Frank Joseph maarufu kwa jina la chui, mwengine ni Henry Benedict maarufu kwa jina la panya, hawa ni wanafunzi maarufu na wengine, na mwanamke pekee anaitwa Paskazia Joseph mwanafunzi wa kidato cha tatu, huyu mwanafunzi ana simu, simu ndio anaitumia kupanga mipango amekamatwa na simu na meseji mbalimbali zinazohusiana na uchomaji wa hapa shuleni,” amesema Kamanda Mwaibambe.

Aidha, Kamanda Mwaibambe ameeleza kwamba kutokana na utovu wa nidhamu wa wanafunzi hao wa kutwa shuleni hapo, bodi iliazimia kuondoa wanafunzi wa kutwa ndipo wakapanga njama za uchomaji wa shule hiyo.

“Mpango wa serikali ni ku-phase out wanafunzi wa kutwa kutokana na matatizo ya miaka na miaka ya shule hii ikiwemo kuchomwa fensi, hao waliobakia ambao ni kidato cha 3 na 4 ambao wapo mwishoni kuondolewa ndio wakapanga mpango kwamba tarehe 5 watawakomesha wananfunzi wa bweni,” amesema Kamanda Mwaibambe.