Ijumaa , 9th Mei , 2014

Wananchi   na  viongozi  wa  jamii   za  Wamasai  na  Wasonjo  wilayani  Ngorongoro  mkoani   Arusha  wamekubaliana kumaliza mgogoro wa siku nyingi ulipo baina ya jamii hizo

Waziri Mkuu Mizengo Pinda akiwa ziarani wilayani Ngorongoro alipokwenda kufanya mkutano na watu wa jamii za wamasai na wasonjo Septemba, 2013

Wananchi   na  viongozi  wa  jamii   za  Wamasai  na  Wasonjo  wilayani  Ngorongoro  mkoani   Arusha   wamesema  wako  tayari  kuwafichua  watu   wanaoingiza  na  kuuza  silaha  za  kivita  na  risasi  zake  katika  maeneo  yao   ambazo  zimekuwa  zikitumika  kuua  watu  wasio  na  hatia. 

Wananchi  hao wameyasema  hayo  katika  kikao   maalumu  cha  usuluhishi  wa  mgogoro   wa  muda  mrefu   miongoni  mwa  jamii  hizo  kilichoshirikisha  viongozi   wa  ngazi mbalimbali   wakiwemo  wa  serikali, dini  na viongozi  wa  mila   ambao   madiwani  wa  kata   za  Samunge na  Olorieni   wamelishwa  kiapo  cha  kimila  cha  kusimamia   amani  katika  eneo  hilo.

Akizungumza  katika  kikao hicho  katibu  mwenezi  wa  CCM  mkoa  wa  Arusha  aliyekuwa  mgeni  rasmi   Joseph Issack  amewataka viongozi  wote  wa  chama  na serikali  kuacha  kuwafumbia  macho   watu  wanaochezea  amani  na  diwani  atakayebainika  kuchochea  mauaji    atavuliwa  madaraka

Baadhi ya  wazee  wa  mila  wa  jamii  hizo  wameendelea  kuitaka  serikali  kuwa  macho  kwani  wapo  baadhi  ya   watu   wanaotaka  kutumia  tofauti  za  jamii  hizo  kutaka  kuvunja  amani   kwani  licha ya  kuwa  tofauti  zao  zilianza  zamani  tangu  enzi  za  aliyekuwa  waziri  mkuu   hayati  Edward  Sokoine   walikuwa  wanazimaliza  kwa  mazungumzo  na   wala  sio  kwa  kutumia  silaha  za  kivita .

Mgogoro huo   wa  ardhi   unadaiwa  kuwa  umeanza  mwaka  1975  na umekuwa  ukiibuka  mara  kwa  mara  na  kupoa  hasa  wakati  msimu  wa  kilimo   na kusuluhishwa  kwa  njia  za  mazungumzo bila  mapigano  wala  umwagaji  wa  damu    lakini   miaka  ya hivi  karibuni  umekuwa  ukisababisha  mapigano   tena  ya  kutumia  silaha  za  kivita  na  umesababisha  vifo na uharibifu  mkubwa  mali.