Jumatano , 12th Jun , 2024

Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego amemwagiza Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Iramba kuchukua hatua haraka za kuwakamata na kuwachukulia hatua wananchi wanaowatishia maisha walimu wa shule ya sekodari Mtekente mkoani humo.

RC Dendego amesema kuwa anataka kuona watumishi waliopo mkoani Singida wanafanya kazi kwa amani bila kusumbuliwa na mtu yeyote na atakayewasumbua basi lazima awajibishwe kwa kuchukuliwa hatua za kisheria.

Aidha Dendego, amekataa kuzindua bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya sekondari Mtekente iliyopo wilayani Iramba baada ya kubaini kuwa ujenzi wa bweni pamoja na jiko yaliyojengwa kwa zaidi ya shilingi milioni 180 yamejengwa chini ya kiwango.

Amesema ujenzi huo wa bweni umejengwa vizuri lakini umaliziaji ndio mbovu katika maeneo mbalimbali ikiwemo kwenye kuta na vyoo hivyo kazi ya maboresho lazima ifanyike haraka kabla ya wanafunzi kurejea mashuleni.