Jumanne , 16th Feb , 2016

Serikali imesema italipa fedha zote zinazodaiwa na wakandarasi nchini kabla ya kuanza kwa mwaka mpya ya fedha wa serikali hatua ambayo imeelezwa kuongeza kasi katika ujenzi wa miradi mingi ya barabara na madaraja ambayo ujenzi wake ulisimama.

Waziri wa ujenzi,uchukuzi na mawasiliano Mh. Prof Makame Mbarawa akizungumza na Mkandarasi hayupo pichani

Hayo yamesemwa na waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano Mh. Prof Makame Mbarawa baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Bulamba-Kisorya wilayani Bunda na ile ya makutano Butiama hadi Mugumu wilayani Serengeti,ambapo amesema wakifanya hivyo itawaondolea adha wakandarasi wanayoipata kutoka katika vyombo vya fedha.

Prof. Mbarawa amesema licha ya serikali ya awamu ya tano kurithi deni la wakandarasi la zaidi shilingi trioni moja lakini hivi sasa deni hilo limeanza kulipwa kwa kasi kubwa na kwamba hadi mwezi june mwaka huu kiasi cha shilingi bilioni 800 kitakuwa kimelipwa kwa wakandarasi.

Waziri Mbarawa ameongeza kuwa barabara ya Makutano - Musoma kupitia Butiama hadi Serengeti, ujenzi wa barabara hiyo utajengwa kwa kiwango cha lami utafanyikakama ulivyopangwa licha ya vikwazo vingi kutolewa na kwamba uamuzi huo utafungua fursa za kibiashara na kurahisisha mawasiliano kati ya mikoa ya kanda ya Kaskazini mwa nchi na ile ya kanda Ziwa Victoria.

Hata hivyo baadhi ya wakandarasi wamepongeza uamuzi huo wa serikali wa kuanza kulipa madeni hayo kwani wamesema kucheleweshwa kwa malipo hayo kumewaongezea riba kubwa za mikopo waliyokopa kutoka vyombo vya fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo.