Jumanne , 30th Jun , 2015

Serikali imesema itawafungulia mashitaka waajiri wote ambao hawawakati pesa waajiriwa wao walionufaika na mikopo ya elimu ya juu kwa ajili ya kurejesha mikopo hiyo katika bodi ya mikopo ya elimu ya juu.

Waziri wa kazi na ajira Mh. Gaudensia Kabaka ametoa tahadhari hiyo leo bungeni mjini Dodoma wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa viti maalum Mh. Christowaja Mtinda kwa niaba ya waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi.

Kabaka amesema sheria iliyoanzisha bodi ya mikopo inawataka waajiri wote wa sekta binafsi kuwakata waajiriwa wao katika mishahara na kuzipeleka pesa hizo bodi ya mikopo kwahiyo kutofanya hivyo ni kwenda kinyume cha sheria, na kwamba tayari kuna baadhi ya waajiri ambao tayari wamekwisha funguliwa mashitaka, na wengine kuhukumiwa.

“Kuna kesi ziko mahakamani na nyingine zimekwishaamuliwa, waajiri wote ambao hawatimizi agizo hilo la sheria watashitakiwa, na mpaka sasa kuna baadhi ya kesi zimekwisha tolewa uamuzi” Amesema Kabaka bila kutaja idadi ya kesi zilizo mahakamani wa la zile zilizoamuliwa.

Kwa upande mwingine mbunge wa Kasulu mjini Moses alitaka kujua hatma ya wanufaika wa mikopo hiyo ambao bado hawajapata ajira, ambapo Mh. Kabaka amesema kwa wale ambao hawajapata kazi watoe taarifa bodi ya mikopo kuwa hawajapa ajira ili wasisumbuliwe kudaiwa na bodi.

"Ambao hawajapa ajira wanatakiwa watoe taarifa kuwa hawajapata ajira ili wafahamike na wasisumbuliwe kudaiwa"