Alhamisi , 18th Sep , 2014

Kundi la vijana wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi 24 nchini Tanzania limetajwa kuwa ndilo linaloongoza kwa maambukizi ya virusi vya ukimwi hali inayochangiwa na vijana wenyewe kutotumia kondomu wakati wa kujamiiana.

Mkurugenzi wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi nchini Tanzania, Dkt Fatma Mrisho.

Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na mratibu wa mipango maalum kutoka tume ya kudhibiti ukimwi nchini Tanzania TACAIDS Bw. Renatusi Kihongo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya hali ya ukimwi nchini.

Bw. Kihongo ameyataja makundi makubwa ya vijana ambayo yamepata maambukizi ya ukimwi kuwa ni pamoja na kundi la vijana wanaojidunga, vijana wanaofanya ngono kinyume na maumbile pamoja na kundi la watu wanaofanya biashara ya ngono ambapo mkoa wa Njombe unaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu walioathirika na virusi vya ukimwi kwa nchi nzima.

Wakati huo huo, Mamlaka ya Elimu nchini Tanzania TEA imetumia zaidi ya shilingi bilioni 11 katika kipindi cha miaka 10 kwa ajili ya kutoa ufadhili wa kununulia vitabu vya kiada kwa shule za sekondari hapa nchini.

Afisa uhusiano wa TEA Silvia Lupembe amesema hayo jijini Dar es salaam wakati alipokuwa akizungumza na East Africa Radio juu namna mamlaka hiyo inavyosaidia katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa vitabu kwa shule za sekondari nchini.

Amesema TEA inatambua changamoto zilizopo kwa sasa katika sekta ya elimu hasa ya upungufu wa madawati, upungufu wa vitabu vya kiada pamoja na upungufu wa vyumba vya maabara hivyo mamlaka hiyo itahakikisha inasaidia kupunguza matatizo hayo kwa lengo la wanafunzi waweze kupata elimu iliyo bora.