Alhamisi , 6th Jun , 2024

Watu wawili wamepoteza maisha baada ya kufukiwa na udongo wakati wakiendelea na shughuli za uchimbaji wa madini katika machimbo yasiyo rasimi  eneo la magenge wilayani na mkoani Geita.

Baadhi ya Wananchi na Wachimbaji Wadogo Wakiwa Eneo la Tukio

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Afisa Zimamoto na Uokoaji mkoa wa Geita Wambura Fide amesema tukio la watu hao kufukiwa na udongo lilipotokea ni eneo lililokatazwa kuendesha shughuli za uchimbaji kutokana eneo hilo kutokuwa na usalama.

"Watu wawili wamefukiwa na kifusi na tayari ndugu wao wamewatambua na watu hao wamejulikana kama Rashidi Twangale (33) mkazi wa Nyakayondwa wilayani Chato, Msumbwa na alikuwa fundi matimba na mchimbaji mdogo mdogo wa pili aliyetambuliwa ni Masunga Nyangota, Msukuma mkazi wa Bariadi"

"Wito wangu kwa wananchi wa kijiji hiki eneo hili sio rasimi kwaajili ya uchimbaji wananchi wanapowaona hawa wazamiaji au Manyani kwenye eneo hili basi watoe taarifa kwa mamlaka husika ili wachukuliwe hatua za kisheria" Wambura Fide, Afisa Zimamoto na Uokoaji mkoa wa Geita

Uongozi wa Kata ya Magenge umewataka wamiliki wa leseni za uchimbaji wa madini katika maeneo yao kubainisha maeneo ya kufanyia kazi na maeneo ambayo yamekatazwa kwani uongozi ulikuwa hauna taarifa kama eneo hilo limekatazwa.

"Pamoja na Tukio hili lililojitokeza lakini wananchi wameumia sana kwasababu wenye leseni wamekuja kujitokeza baada ya tukio hili kutokea cha kuwaomba wenye leseni eneo hili ambalo wenzetu wamepoteza maisha walete sikaveta wafukie mashimo hayo ili wananchi waache kuingia humo" Edward Misungwi, Diwani wa Kata ya Magenge

"Hawa wenye leseni baada ya kusikia kwenye eneo lao kumetokea maafa ndo wakajitokeza na kuja na barua ya kukataza eneo hilo kuwa limefungwa arafu barua imenadikwa tarehe 4 siku ya tukio la siku zote sisi kama viongozi wa kijiji tulikuwa hatujui mmiliki wa leseni ya hapa ni nani" Matias Deo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Magenge

 "Tunaomba Serikali yeyote anayenda kuchukua leseni afike kwanza kwenye uongozi wa serikali ya kijiji vile vile na wenye mashamba wamjue lakini pia aweke na wasimamizi wa kulinda eneo hili tofauti na hapo matukio kama haya yataendelea" Samwel Machibya, Mkazi wa Magenge

 EATV Imefanikiwa kuzungumza na Abdul Joseph Stansilausi ambaye ni Mmiliki wa leseni hiyo amesema kabla ya kutokea kwa ajali hiyo alikuwa ameshatoa taarifa kwa viongozi husika.

"Kabla ya tukio hili nilikuja nikasavei mazingira ya leseni yangu nikaona hali sio nzuri watu wanaendelea kuchimba nikaenda kwa mtendaji nikakuta katoka yupo katoro nikampigia simu akasema ni kweli tupo tunafanya utaratibu wa kuwaondoa lakini pia lile eneo ni la utafiti bado tupo kwenye utafiti kwa sasa sifaidiki na chochote pale" Abdul Joseph Stansilaus