Jumanne , 20th Aug , 2019

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda, amewataka watanzania kuhakikisha wanatumia fursa mbalimbali zilizotangazwa kupitia mkutano wa Jumuiya ya Maendeleo ya Wakuu wa nchi Kusini mwa Afrika (SADC).

Paul Makonda

Makonda ameyabainisha hayo leo Agosti 20, wakati akimpongeza Rais John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa nchi 16, zinazounda jumuiya ya  SADC kwa madai ya kwamba kuna watu wamekuwa wakimhoji wao watanufaika vipi na SADC.

''Ukisikiliza vizuri hotuba za Rais Magufuli lazima utaziona fursa nyingi sana, sasa Rais aongelee namna ya kupata soko lako angalau uuze mahindi au Njegere, fursa ya Kiswahili nayo hujaiona? sasa wewe huwezi kufanya ya kiuchumi, huwezi kufanya ya kibiashara basi olewa angalau ile ya kuoa na kuolewa nayo huioni?, Rais hawezi kuja kukuwekea pesa mfukoni'' amesema Makonda.

Aidha Makonda amewataka wananchi,  kuendelea kudumisha suala la usafi kama ilivyokuwa kipindi cha mkutano wa viongozi wakuu wa SADC, uliohitimishwa Agosti 18.