Jumatano , 6th Apr , 2016

Tanzania imeshaandaa timu ya uchunguzi kwenda nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC,ili kuchunguza ripoti za unyanyasaji wa kingono uliodaiwa kufanywa na walinda amani wa Tanzania kwenye Ujumbe wa Umoja wa Mataifa MONUSCO.

Majeshi ya MONUSCO yanayoongozwa na Wanajeshi Kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ

Ujumbe wa Kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa mjini New York umetangaza hilo baada ya kikao na Idara ya Usaidizi kwa ajili ya vitengo vya Umoja wa Mataifa katika nchi mbalimbali.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Farhan Haq, amewaambia leo waandishi wa habari kwamba Umoja wa Mataifa unaishauri mamlaka za Tanzania kuendesha uchunguzi huo kwa ushirikiano na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Usimamizi wa masuala ya ndani (OIOS).

Bw. Haq ameongeza kwamba miongoni mwa wanawake 11 wanaodaiwa kuwa wahanga wa ukatili huo, sita walikuwa wenye umri wa chini ya miaka 18.

Aidha, ameeleza zaidi kwamba saba wameshazaa na wengine wanne bado wako na ujauzito, na wote sasa hivi wanasaidiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF ambalo limepeleka timu maalum kwa ajili yao.

Tuhuma hizo zilitangazwa jumatatu hii na msemaji wa Umoja wa Mataifa.

Askari wote wa kikosi cha Tanzania nchini DRC wamezuiliwa kambini uchunguzi ukiendelea.