Ijumaa , 11th Mar , 2016

Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa - UNDP limetoa ripoti ya hali ya maendeleo ya mwanadamu kwa mwaka uliopita, ripoti inayoonyesha kuwa Tanzania bado inakabiliwa na changamoto ya kuwa na mazingira bora ya kazi na ajira zenye staha.

Naibu Waziri wa Kazi, Ajira, vijana na walemavu mheshimiwa Anthony Mavunde

Changamoto hizo kwa mujibu wa ripoti hiyo, ndiyo zinazopaswa kushughulikiwa iwapo serikali inataka kuboresha hali ya maisha ya watu wake na hatimaye kufikia dira ya maendeleo ya taifa ya mwaka 2030.

Mwakilishi mkazi wa UNDP nchini Bw. Alvaro Rodriguez amesema hayo na kufafanua kuwa kuna uhusiano wa karibu kati ya ajira bora na maendeleo ya watu hivyo kuna haja ya serikali kuwa na mipango inayotekelezeka ya kuboresha ajira na mazingira ya kazi kwa watu wake.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Kazi, Ajira, vijana na walemavu mheshimiwa Anthony Mavunde amewataka waajiri kuheshimu sheria za kazi kwa kutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi wao huku wakitambua kuwa amani na usalama ndio njia pekee inayoleta tija na ufanisi maeneo ya kazi.

Naibu Waziri Mavunde amesema wizara yake inaendelea na zoezi la ukaguzi wa maeneo ya kazi ili kuona kama waajiri wanafuata sheria ya kazi inayowataka kutoa mikataba ya ajira pamoja na kuweka mazingira bora na salama ya kazi.