Alhamisi , 16th Apr , 2015

Wizara ya Uchukuzi nchini Tanzania imewasimamisha kazi viongozi wakuu watano wa Kampuni ya Reli Tanzania TRL, kufuatia kuingizwa na kulipwa kwa manunuzi ya mabehewa mabovu ili kupisha uchunguzi.

Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Samuel Sitta

Akitangaza kuwasimamisha viongozi hao leo jijini Dar es salaam, Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Samuel Sitta amesema wizara itaunda kamati itakayoongozwa na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali CAG, akishirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU, Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma PPRA pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mhe. Sitta amesema miongoni mwa viogozi hao watakaochunguzwa kwa majuma matatu kuanzia April 20 mwaka huu ni pamoja na Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo, Kipalo Kisamfu, mhandisi mkuu wa mitambo wa kampuni, Ngosomwile Ngosomiles pamoja na mkaguzi mkuu wa ndani wa kampuni, Jasper Kisiraga.