Jumatano , 13th Apr , 2016

Serikali ya Tanzania imewashauri wawekezaji kutoka Oman kuongeza nguvu ya uwekezaji katika viwanda vya sukari ili kusaidia viwanda hivyo kuzalisha sukari ya kutosha sambamba na bidhaa nyingine zitokanazo na mabaki ya miwa ikiwemo amira.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan

Kauli hiyo imetolewa hii leo na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan wakati akifungua mkutano wa kibiashara baina ya wafanyabiashara wa Oman na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wenye lengo la kuangalia fursa za uwekezaji na kuangalia maeneo ya kushirikiana ili nchi hizo mbili ziweze kufanya kazi kwa pamoja.

Alisema ili kushirikiana katika biashara baina ya mataifa hayo mawili ni vyema serikali ya Oman ikajikita katika kuongeza nguvu katika viwanda na kuzalisha sukari ya kutosha sambamba na bidhaa nyinginezo zitokanazo na mabaki ya miwa.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage amesema kupitia mkutano huo watajadili namna ya kuzalisha bidhaa mahususi ambazo zitasafirishwa nje ya nchi ikiwemo Omani, zenye lengo la kuwainua pia wajasiriamali wadogo nchini.