Ijumaa , 25th Nov , 2016

Makamu wa Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema serikali itaendelea kuviimarisha vyuo vya ufundi stadi nchini –VETA- ili viweze kutoa wahitimu bora ambao watakidhi katika soko la ajira hasa kwenye viwanda vilivyopo na vitakavyojengwa nchini.

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan

 

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa kauli hiyo leo wakati anazungumza na uongozi wa kiwanda cha A to Z kilichopo mkoani Arusha katika ziara yake ambayo imeingia siku ya pili ya kutembelea viwanda mbalimbali mkoani humo ili kujua changamoto zinazokabili viwanda hivyo na serikali kuzitafutia ufumbuzi.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amesema serikali imetenga fedha za kutosha zitakazotumika kuviimarisha vyuo vya Veta ili viweze kutoa mafunzo bora yatakayosidia vijana kufanya kazi zao kwa ufanisi wa hali ya juu pindi watakapoajiriwa au kujiajiri wenyewe.

Kuhusu maslahi kwa wafanyakazi wa Kiwanda cha  A to Z, Makamu wa Rais  ameutaka uongozi wa kiwanda hicho kulinda na kutetea haki za wafanyakazi kwa kutoa maslahi mazuri ambayo yatawezesha wafanyakazi hao kufanya kazi kwa bidii.

Makamu wa Rais pia amesisitiza usawa katika ulipaji wa mishahara kwa wafanyakazi wa ndani na wa nje ya nchi walioajiriwa kwenye kiwanda hicho ili kuondoa tofauti za mishahara hali ambayo ijenga motisha kwa wafanyakazi.

Kiwanda cha A to Z kilichopo eneo la Kisongo mkoani Arusha kimeajiri zaidi ya wafanyakazi 7500 ambapo asilimia 80 ya wafanyakazi wote ni wanawake.

Amewahimiza wawekezaji kote nchini walipe kodi za serikali mapema kodi ambazo zitatumika   kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.