Alhamisi , 4th Sep , 2014

Serikali ya Tanzania imetakiwa kuwasaidia vijana kwa kuwapa miongozo ikiwa pamoja na kuwadhamini katika upatikanaji wa fedha ili kupunguza ongezeko la tatizo la ajira nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Masuala ya Kiuchumi na Kijamii ESRF Dkt Bohela Lunogelo (wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wizara ya Fedha Dkt Servacius Likwelile (katikati).

Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF) Dkt. Bohela Lunogelo wakati wa uwasilishaji wa ripoti ya awali kuhusu suluhisho la tatizo la ajira kwa vijana.

Dkt. Lunogelo amesema tatizo la ajira limewasababishia vijana wengi kuwa tegemezi kwa kushindwa kubuni mbinu za kujikwamua na ugumu wa maisha jambo ambalo hurudisha nyuma juhudi zao katika kujikwamua kimaendeleo.

Kwa upande wake msimamizi wa utafiti huo Dkt. Jojina Olesaibulu amesema utafiti huo umehusisha mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza na Morogoro ambapo wengi wa vijana wameleza kuwa wanakumbwa na changamoto ya kukosa uzoefu wa kazi ikiwemo ukosefu wa elimu kuhusiana na kazi zinazotangazwa.