
Rais wa zamani wa Ufaransa Nicolas Sarkozy leo ameanza kutumikia kifungo cha miaka mitano gerezani baada ya kuhukumiwa kwa uhalifu wa kula njama ya kufadhili uchaguzi wa mwaka 2007 kinyume na sheria kwa kutumia fedha zilizotoka kwa aliyekuwa kiongozi wa Libya Muamar Gaddafi.
Bwana Sarkozy mwenye umri wa miaka 70 aliwasili leo asubuhi katika jela la La Sante mjini Paris akisindikizwa na mkewe Carla Bruni na kushangiliwa na wafuasi wake walioimba wimbo wa taifa. Kupitia ukurasa wake wa X,Kiongozi huyo amedai ni muathiriwa wa chuki na visasi na kuongeza kuwa anayefungwa leo gerezani sio rais wa zamani wa Ufaransa bali mtu asiye na hatia.
Amekuwa akikanusha mara kwa mara kuhusika na makosa yoyote yanayohusiana na ufadhili wa uchaguzi wa 2007.
Sebastien Cauwel,mkuu wa gereza atakalofungwa bwana Sarkozy amesema kiongozi huyo atafungwa kwenye seli yake pekee, tofauti na wafungwa wengine lakini ataweza kutumia uwanja wa kufanyia mazoezi mara mbili kwa siku akiwa pekee yake kwasababu za kiusalama.
Sarkozy ambaye alikuwa Rais wa Ufaransa kati ya mwaka 2007 hadi 2012,atakuwa rais wa zamani wa Ufaransa kufungwa jela tangu Marshal Philipphe,aliyekuwa kiongozi wa Ufaransa na mafungamano na utawala wa kinazi kufungwa baada ya vita vya pili vikuu vya dunia.